BARNABA KUTOKA NA STAILI MPYA YA UIMBAJI ,UVAAJI PAMOJA NA MITINDO YA NYWELE
Msanii nyota anayetingisha kwenye anga za muziki wa kizazi kipya nchini Barnabas Elias ‘Barnaba’ yuko mbioni kuzindua staili yake mpya ya uimbaji inayoambatana na muonekano mpya wa mavazi pamoja na mtindo wa nywele ambayo atatumia kwa ajili ya kutoa burudani kwa mashabiki wake
Msanii huyo alieleza kuwa lengo lake ni kuwa na muonekano wa tofauti na wasanii wengine kwani anachojali yeye ni ubunifu zaidi
Pamoja na kuwa na nembo inayomtambulisha kazi zake kiujumla kwa mashabiki na wadau wake wa muziki na kuweza kuupaisha muziki ndani na njee ya mipaka ya Tanzania
Barnaba aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hii juu ya kuzindua staili yake ya nywele pamoja na uvaaji
“Watu washazoea kumuona Barnaba na aina moja ya nywele sasa wataniona niko tofauti kuanzia nywele mpaka aina ya mavazi nitakayokuwa nikivaa pamoja na viatu” alisema
Barnaba alisema kuwa uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika hivi karibuni katika hoteli ya Serena ambapo atatoa mialiko kwa watu maalum
Aliongezea kuwa staili hiyo na muonekano huo mpya ameubuni mwenyewe ili kuweza kuongeza amasa kwa wadau na mashabiki wake wa muziki, kwani mashabiki wanapenda msanii ambaye ni mbunifu na si Yule anayeiga kazi za wenzie
Aliongezea kuwa katika uzinduzi huo utasindikizwa na waimbaji nyota kutoka kundi la Nyumba ya Kukuza Vipaji ya THT na makundi mengine pia atatumia fursa hiyo kuzitambulisha nyimbo zake mpya ambazo hazijawahi kusikika








