Google PlusRSS FeedEmail

MAHAKAMA YAKUBALI ALIYEKUWA MWANAUME AWE MWANAMKE

                                
MAHAKAMA Kuu imeamuru Baraza la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNEC), libadilishe jina cheti cha mlalamikaji ambaye amekuwa akipigana atambuliwe kuwa mwanamke.


Jaji Weldon Korir jana Jumanne aliagiza KNEC impe cheti kipya Bi Audrey Mbugua kikiwa na jina jipya lililochapishwa katika gazeti rasmi la serikali.
Mlalamikaji, ambaye awali alitambuliwa kwa jina Andrew Ithubu Mbugua, alibadilisha jina lake kuwa Audrey Mbugua.

Bi Mbugua aliishtaki KNEC kwa kukataa kubadilisha jina lake na kuondoa neno “mwanaume” katika cheti chake kuonyesha kuwa ni “mwanamke” hata baada ya kuonyesha gazeti rasmi la serikali lililochapisha mabadiliko kwenye jina lake.
Jaji Korir ameipa KNEC siku 45 kutayarisha cheti kipya na kumpa Bi Mbugua kikiwa na jina lake jipya.

Jaji aliamuru herufi “M” ambayo inamaanisha “mwanaume” iondolewe katika cheti nambari 1855399 ambacho Bi Mbugua alipewa na KNEC kwa jina la Ithubu Andrew Mbugua.
Jaji aliamuru cheti hicho kitolewe upya kwa jina jipya la “Audrey Mbugua” bila herufi “M” (mwanaume) ama “F” (mwanamke) akisema herufi hizo haziongezi maana au thamani yoyote kwa cheti hata zikitolewa.

“Mlalamikaji ni mwanamke ambaye amegubikwa kwenye mwili wa mwanamume ... maumbile ya kike ndani yake yanazidi yale ya kiume na sina budi kuamuru mlalamikaji ajihisi mkamilifu,” alisema Jaji Korir.

Jaji alisema katiba inaelezea wazi kwamba “kila mtu anatakiwa kuchukuliwa kwa heshima na lazima kipengee hiki kimfaidi mlalamishi kabisa.
Kutokitekeleza kwa manufaa yake ni kukiuka haki zake.

Alisema kama Audrey atajihisi “mzima” ni lazima akubalike jinsi alivyo na kumnyima haki ya kubadilisha jina lake ni kukiuka haki zake na uhuru aliopewa na katiba.A

Wakili wa Audrey, Bw Colbert Ojiambo, aliIambia mahakama kuwa mlalamikaji alizaliwa jinsia yake ikiwa na utata na amekuwa akitibiwa katika hospitali moja Nairobi.
Jaji Korir alisema ameangalia kesi nyingine za aina hiyo na kufikia uamuzi kwamba zote zinaegemea haki na heshima kwa binadamu.

“Mlalamikaji aliwasilisha mahakamani gazeti rasmi la serikali lililochapishwa Januari 19, 2012 ambapo jina lake limebadilishwa kuwa Audrey na Mkuu wa Sheria akasema hapingi kubadilishwa kwa jina lake,” akasema jaji.

Alisema sheria nambari 9(1) ya mitihani inasema cheti kinachotolewa na KNEC kinafaa kuonyesha jina la mwanafunzi, nambari ya usajili na masomo aliyofanya, alama alizopata na kwamba kinatolewa kwa utaratibu fulani.

Jaji Korir alisema sheria inaruhusu mabadiliko kufanyiwa cheti na kwamba herufi ya kuonyesha jinsia haina maana wala si lazima iwepo.

This entry was posted in

Leave a Reply

    Powered By Blogger

    Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below...

    Get This SpiceUpBlogging