Google PlusRSS FeedEmail

TWANGA, KALA JEREMIAH, BEN POL KUTUMBUIZA TAMASHA LA 'WORLD MUSIC DAY IJUMAA


Tamasha la muziki la kimataifa ambalo hufanyika kila mwaka la ‘World Music Day’ linafanyika leo (Ijumaa) katika viwanja vya posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam ambapo wanamuziki Kala Jeremiah, Ben Paul, bendi ya Twanga pepeta na wengineo wanaotamba katika tasnia ya muziki nchini watalipamba tamasha hilo.

Tamasha hilo ambalo limeandaliwa na Umoja wa Ulaya wa taasisi za utamaduni (EUNIC) zikiwamo Aliance France-Dar es Salaam, Goethe Institut-Tanzania na British Council linalenga kutoa fursa kwa wanamuziki wakongwe na wachanga kukutana katika jukwaa hilo la kimataifa kutoa burudani hiyo kwa wapenzi na mashabiki wa muziki.

Mratibu wa Tamasha hilo ambalo limedhaminiwa na Fasjet, Abel Shuma ambaye pia ni Mratibu wa Shughuli za Utamaduni Alliance France Dar es salaam amewataja wasanii watakaotumbuiza katika tamasha hilo kuwa ni pamoja na Msanii wa Reggae nchini Jhiko Man, Barnaba na bendi yake, Ben Paul na Twanga Pepeta

Wengine ni Msanii bora wa mwaka na msihindi wa tuzo tatu za KTMA Kala Jeremiah, Godzila, Super Maya Baikoko, Makini Kids na wengine wengi ambao watajumuika kwa pamoja kunogesha tamasha hilo ambalo hufanyika Juni 21 kila mwaka katika nchi 116.

Shuma amesema hakutakuwa na kiingilio katika tamasha hilo ambalo linatarajiwa kuanza majira ya saa kumi na moja jioni na hivyo kuwaomba wapenzi na mashabiki wa muziki kujitokeza kwa wingi katika tamasha hilo linalodhaminiwa na Fastjet, Balozi za Ufaransa na Ujerumani, kinywaji cha Pepsi na Total.

Kala Jeremiah analielezea onyesho hilo kama mazao ya kazi nzuri aliyoifanya katika muziki wake “Nimepata faraja sana kualikwa kutumbuiza kwenye world music day, inaonyesha ni kwa jinsi gani muziki wangu unakubalika na kutambulika kitaifa na kimataifa”.

Shirika la ndege la Fastjet kupitia kwa Afisa Masoko Mtendaji Lucy Mbogoro linajivunia kudhamini tamasha hilo likitumia nafasi hiyo kurejesha shukran kwa Watanzania kwa mchango wao mkubwa katika shirika hilo kwa kuchagua kutumia huduma zake za usafiri wa anga.

Mbogoro anasema “World Music Day ni fursa nzuri ya kukutana na wadau wetu kwakuwa tamasha litawakutanisha watu wa mataifa mengi watapata kujua huduma zetu katika wakati huu tunaoelekea kuanzisha safari za ndege za kimataifa katika nchi za Afrika Kusini, Zambia na Rwanda”


This entry was posted in

Leave a Reply

    Powered By Blogger

    Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below...

    Get This SpiceUpBlogging