Shirika la habari la televisheni la NBC nchini Marekani, limetangaza Jumanne kuwa limemsimamisha kazi kwa miezi sita bila malipo mtangazaji wake wa habari Brian Williams kwa kuongeza chumvi katika taarifa aliyoripoti juu ya vita vya Iraq.
Williams mwenye umri wa miaka 55 ambaye ameomba radhi hadharani, hivi sasa yuko chini ya uchunguzi unaofanywa na kituo hicho cha televisheni. Mwishoni mwa wiki iliyopita alitangaza kujiondoa kwenye matangazo ya jioni ya shirika hilo,yanayotazamwa sana na Wamarekani.
Katika taarifa ya maandishi mkuu wa shirika hilo Steve Burke amesema Brian ameweka imani ya shirika la NBC hatarini kwa mamilioni ya wamarekani waliokuwa wanafuatilia habari kuu za kila jioni kutoka kwa shirika hilo. Burke, alisema aliyofanya Brian, hayana kisingizio na kwamba hatua ya kumsimamisha kazi ni hatua kubwa na inayostahili